Saturday, April 2, 2016

M’kiti halmashauri Arusha, wenzake 4 kortini kwa tuhuma za kujeruhi






MWENYEKITI wa Halmashauri ya Arusha, Noah Lembris

 
MWENYEKITI wa Halmashauri ya Arusha, Noah Lembris na wenzake wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha kwa tuhuma za kujeruhi na kuharibu mali.
Washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana mbele ya Hakimu Mkazi Gwanta Mwankuga na kusomewa mashtaka yanayowakabili katika kesi namba 83 na 84 za mwaka 2016 .

Pamoja na Mwenyekiti huyo wa Halmashauri ambaye ni Diwani wa Kata ya Oltumet kupitia Chadema, watuhumiwa wengine ni William Samwel, Rafael Ngosira, Loserian Solomon na Lucas Lairumbe.

Akisoma mashtaka hayo, Mwanasheria wa Serikali Riziki Riziki alidai mahakamani hapo kuwa mshatakiwa wa kwanza Noah Lembris na Wiliam Samweli kwa pamoja Septemba 27, mwaka jana katika eneo la Olorien wilayani Arumeru walidaiwa kuchoma moto nyumba ya mkazi wa eneo hilo Peter Kambey.

Katika shtaka la pili linalowakabili watuhumiwa wote inadaiwa Februari 29, mwaka huu wanadaiwa kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili Peter Kambey wakati akiwa shambani kwake na kumsababishia maumivu makali.

Watuhumiwa wote walikana mashtaka yanayowakabili na waliachiwa kwa dhamana hadi Aprili 14, mwaka huu ambapo kesi hiyo itatajwa tena mahakamani hapo. Awali kabla ya kupandishwa mahakamani na kusomewa mashtaka hayo, watuhumiwa hao walikuwa katika mgogoro wa kugombea shamba lenye ukubwa wa ekari 6 mali ya ajuza Ndetiai Megaro (84) mkazi wa kijiji cha Ilkiushi wilayani Arumeru.

Mgogoro huo uliodumu kwa takriban miaka 12 unatokana na baadhi ya viongozi wa kisiasa akiwemo Mwenyekiti Lembris kujaribu kudhulumu shamba hilo kwa kuhamisha umiliki kutoka kwa bibi huyo na kudai kuwa ni eneo la kijiji cha Ilkiushi.

Kitilya, wenzake wawili kortini




Kamishna Mkuu mstaafu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya (wa pili kushoto), Shose Sinare (wa pili kulia) na Sioi Sumari (kushoto) wakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam jana. (Na Mpigapica Wetu).


SAKATA la rushwa ya Dola za Marekani milioni 600, linalohusisha Benki ya Standard ya London Uingereza, jana lilichukua sura mpya baada ya kufikishwa mahakamani kwa aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya, akikabiliwa na mashitaka mbalimbali, ikiwemo utakatishaji wa fedha.

Washitakiwa wengine waliounganishwa katika kesi hiyo ni pamoja na mrembo wa zamani wa Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Uwekezaji wa Benki ya Stanbic, Shose Sinare na aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Sheria wa benki hiyo, Sioi Graham Solomon. Mashitaka mengine yanayowakabili katika kesi hiyo mbali na kutakatisha fedha, ni pamoja kutumia nyaraka za kughushi na za uongo kujipatia isivyo halali Dola za Marekani milioni 6, sawa na Sh bilioni 12 za Tanzania.

Mbele ya Hakimu Mwandamizi, Emilius Mchauru washitakiwa hao walikana mashitaka hayo na kurudishwa rumande mpaka Aprili 8 mwaka huu, wakati mahakama itakapokutana kusikiliza shauri kuhusu dhamana yao. Upande wa utetezi, ukiwakilishwa na mawakili Dk Ringo Tenga na Semu Anney, waliomba mahakama itoe dhamana kwa wateja wao.

Hata hivyo, upande wa Mashitaka ukiwakilishwa na wanasheria waandamizi wa Serikali; Oswald Tibabyekomya na Christopher Msigwa pamoja na Mwanasheria wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru), Stanley Luwoga walipinga dhamana hiyo kwa madai kuwa kesi za utakatishaji fedha hazina dhamana.

Awali upande wa mashitaka uliieleza mahakama kwamba, katika tarehe tofauti kati ya Agosti 2012 na Machi 2013, katika Jiji la Dar es Salaam, washitakiwa hao watatu walipanga pamoja kwa kushirikiana na watu wengine ambao hawakufikishwa mahakamani hapo, kutenda kosa la kujipatia fedha kwa udanganyifu kutoka serikalini.

Ilidaiwa kuwa kati ya Agosti 2, 2012 katika Makao Makuu ya Benki ya Stanbic Tanzania Limited yaliyopo wilayani Kinondoni, mshitakiwa Sinare akiwa na nia ovu, alighushi taarifa ya maombi ya fedha ya Benki ya Standard ikiwa na tarehe ya Agosti 2, 2012.

Kwa mujibu wa madai hayo, Sinare alieleza katika maombi hayo kuwa Benki ya Standard ya London kwa kushirikiana na Benki ya Stanbic ya Tanzania, watatoa mkopo unaofikia Dola za Marekani milioni 550 kwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa gharama ya asilimia 2.4 ya mkopo huo, wakati akijua kuwa gharama hiyo si kweli.

Mahakama ilielezwa kuwa Agosti 13, 2012, mrembo huyo wa zamani wa Tanzania, aliwasilisha taarifa hiyo ya kughushi katika Wizara ya Fedha iliyopo Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam. Imedai kuwa Septemba 20, 2012 katika Benki ya Stanbic, Sinare alitengeneza barua ya uongo ya kuelezea mkopo huo wa Dola za Marekani milioni 550, ikieleza kuwa Benki ya Standard PLC kwa kushirikiana na Benki ya Stanbic, zitatoa mkopo huo kwa Serikali kama wakikubaliwa
.
Upande huo wa mashitaka uliendelea kudai kuwa, Sinare aliwasilisha barua hiyo ya uongo katika Wizara ya Fedha kwa lengo hilo hilo. Kwa mujibu wa madai hayo, Novemba 5, 2012 katika Benki ya Stanbic jijini Dar es Salaam, washitakiwa wote watatu, wakiwa na nia ovu, walitengeneza makubaliano ya uongo kwa lengo la kuonesha kuwa benki imeipa kampuni ya Enterprise Growth Market Advisors (EGMA) Limited, kazi ya kushughulikia mkopo huo.

Bei ya umeme yashuka

 
 
MAMLAKA ya Udhibiti ya Huduma za Nishati na Maji (Ewura) imepunguza bei ya umeme baada ya kupokea ombi la Shirika la Umeme (Tanesco). Katika maombi yake, Tanesco waliomba kupunguza umeme kwa asilimia 1.1 lakini baada ya Ewura kupitia maombi hayo imepunguza kwa asilimia 1.5 hadi 2.4 kutoka bei ya sasa.

Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi alisema bei hiyo mpya ya umeme, imeanza kutumika jana. Kwa mujibu wa Ngamlagosi, Ewura walifikia hatua hiyo ya kupunguza zaidi ya maombi ya Tanesco, baada ya kukaa na wadau.
Mbali na kushusha bei ya umeme, Ngamlagosi alisema pia baadhi ya gharama ambazo ni tozo ya kuwasilisha maombi ya kuunganishiwa umeme ambayo ilikuwa Sh 5,000 na tozo ya huduma ya mwezi (service charge) iliyokuwa Sh 5,520 kwa wateja wa majumbani ambao wapo katika kundi la T1, pia vimefutwa Ngamlagosi alisema hata marekebisho ya bei za umeme kwa mwaka 2017, yameahirisha mpaka Tanesco itakapowasilisha upya maombi hayo kabla ya Agosti 31, mwaka huu.
“Kutokana na kifungu cha Sheria ya Umeme ya mwaka 2008, kifungu cha 23 (2) na 23 (3), yatakuwepo marekebisho ya bei za umeme kutokana na mabadiliko ya bei za mafuta, thamani ya fedha na mfumuko wa bei. Marekebisho hayo yatafanyika kwa mujibu wa kanuni ya 7 ya urekebishaji wa bei za umeme ya mwaka 2016,” alisema.

Aliongeza kuwa kundi la wateja wadogo wa nyumbani wale wa kipato kidogo ambao wanatumia uniti moja hadi 75, wanatakiwa kwa mwezi kulipa Sh 350 kwa kila uniti inayozidi.

Pia, kwa watu wa majumbani wenye matumizi makubwa wana punguzo la Sh 6 kutoka Sh 298 kwa uniti hadi 292. Kundi jingine lililonufaika na punguzo hilo, limetajwa kuwa ni wafanyabiashara wa kati ambao ni wenye mitambo, hoteli na migahawa ambao wana punguzo la Sh 5 kutoka Sh 200 hadi 195.

Ngamlagosi alifafanua kuwa wateja wa viwandani wamepunguziwa Sh 2 kwa uniti toka Sh 159 hadi 157 na wateja wanaotumia msongo mkubwa wa umeme wana punguzo la Sh 4 kutoka Sh 156 hadi 152 kwa uniti.

Alisema pia Tanesco ilipeleka ombi la punguzo la umeme la mwaka 2017 ambalo walipendekeza bei ya umeme ipungue kwa asilimia 7.9, lakini pendekezo hilo limeahirishwa mpaka hapo watakapowasilisha upya maombi kabla ya Agosti 31, mwaka huu.

Mkwasa arejea Yanga




Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwassa.
 
KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Charles Mkwasa ameitwa kuongeza nguvu katika benchi la ufundi la Yanga kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri wiki ijayo.

Habari zilizopatikana jana kutoka Yanga, zilieleza kuwa tayari Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeshatoa ruhusa ili aweze kuisaidia Yanga kipindi hiki cha kuelekea mchezo huo. “Ni kweli Mkwasa ameitwa kuongeza nguvu, unajua Kocha wa Yanga (Hans Pluijm), anamkubali sana Mkwasa, hivyo wameona aje asaidie wakati huu ambapo hana majukumu Taifa Stars,” kilisema chanzo chetu na kusisitiza kwamba Mkwasa haina maana amejiondoa Taifa Stars.

Mkwasa hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo, wala Ofisa Habari wa Yanga, Jerry Muro na hata Ofisa Habari wa TFF, Baraka Kizuguto. Hata hivyo, TFF iliwahi kutoa taarifa kwamba timu za Yanga na Azam zipo huru kuwatumia makocha wa Taifa Stars, Mkwasa na Hemed Morocco katika maandalizi yao kwa ajili ya michezo ya kimataifa inayowakabili.

Mkwassa alikuwa Kocha Msaidizi wa Yanga kabla ya kuteuliwa kuwa kocha muda wa Taifa Stars katikati ya mwaka uliopita akirithi mikoba ya Mholanzi Mart Nooij aliyetimuliwa baada ya matokeo mabaya ya Stars.

TFF ilisaini naye mkataba wa miezi 18 Oktoba mwaka jana baada ya kuridhishwa na kazi yake, ambapo mkataba huo utamalizika Machi 31 mwakani. Wakati huohuo, Mohammed Akida anaripoti kuwa Pluijm amesema ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ndanda FC juzi utachangia kukiimarisha kikosi chake kwa mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly mwishoni mwa wiki ijayo.
Yanga juzi ilishinda mabao 2-1 katika mchezo wa robo fainali Kombe la Shirikisho, lakini haikuonesha kiwango cha kuvutia kiasi cha mashabiki kuingiwa na hofu kuhusu mchezo wao na Ahly.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Pluijm alikiri timu yake kucheza vibaya, lakini alisema hiyo ni moja ya mikakati yao kuhakikisha wanatunza nguvu za kucheza mechi zingine tatu zinazowakabili ikiwemo ya Al Ahly.

Pluijm alisema huo ni ushindi mkubwa kwao na sasa wanajipanga kushinda michezo miwili ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar na Mtibwa Sugar kabla ya kuikabili Al Ahly Jumamosi ijayo.

Friday, April 1, 2016

Usawa wa kijinsia katika jamii za kitanzania bado ni kizungumkuti




 


Wanafunzi wakisikiliza semina
 
 Bi Fatma Amiry akitoa semina ya jinsia katika ukumbi wa chuo cha uandishi wa habari Arusha

Kulingana na usanyanyasaji wa kijinsia unaoendelea katika maeneo  mbalimbali  nchini,jamii imehaswa kuweka usawa wa kijinsia ili kuweza kutokomeza adha hiyo.
Hayo yamesemwa na  Bi. Fatma Amiry ambaye ni Afisa ustawi wa jamii mkoani Arusha  katika semina  ya  kupinga unyanyasaji  wa kijinsia na maambukizi ya Ukimwi iliyofanyika katika ukummbi wa chuo cha Uandishi wa Habari na utangazaji  Arusha (AJTC).
Ameeleza kuwa  jamii  nyingi  za kitanzania bado zinamitazamo  hasi kuhusiana na suala la usawa  wa kijinsia  kutokana na mila na destuuri walizojiwekea  ambazo  zinaleta migogoro na usnyanyasaji wa kijinsia.
Bi Fatma amesema  jamii inatakiwa ibadilike kulingana na wakati uliopo ili kuweza kuleta usawa huo katika jamii ikiwa ni pamoja na wanawake kurithi mali,kupewa elimu na kutokudharauliwa
“Ni wakati wa mabadiliko katika jamii zetu, maisha ya zamani ni tofauti na sasa hivyo nawaomba watanzania wenzangu waache kunyanyasa jinsia tofauti ili kuweza kutimiza malengo ya haki sawa kwa wote”Alisema Bi. Fatma Amiry
Licha ya hayo pia amewashauri vijana na jamii kwa ujumla  kupima afya  na kuwa  waaminifu kwa wapenzi wao  ili kuweza kupunguza kasi ya maambukizi  ya  virus vya  Ukimwi
Kwa upande wake mkufunzi wa chuo hicho Bw. Lucas Modaha amesema  vijana na wanandoa wajiheshimu na kulinda utu ili kuepuka maambukizi mapya ya VVU

Thursday, March 31, 2016

MWANZA KINARA WATUMISHI HEWA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene

WAKUU wa mikoa 26 ya Tanzania Bara wamekabidhi ripoti za uhakiki wa watumishi hewa katika mikoa yao, ambazo zimeonesha kuwa na watumishi hewa zaidi ya 2,000, huku Mkoa wa Shinyanga ukiwa hauna mtumishi hewa yeyote wakati Mwanza ndio kinara ukiwa na watumishi hewa 334.

Watumishi hao zaidi ya 2,000 wameisababishia serikali hasara zaidi ya Sh bilioni nne, huku mikoa ya Mwanza, Singida, Kigoma, Pwani, Dodoma, Morogoro na Kilimanjaro ikionekana kuwa na idadi kubwa ya watumishi hewa.

Ripoti hizo ziliwasilishwa jijini Dar es Salaam jana na Wakuu wa Mikoa hao kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene ambaye alisema ripoti hizo atazifikisha kwa Waziri mwenye dhamana ya Utumishi kwa ajili ya kuhakikiwa, kabla ya kuwasilisha kwa Rais John Magufuli.

“Nitazipeleka kwa Waziri wa Utumishi ili yeye azifanyie uhakiki na zipitiwe upya…hata kwenye wizara pia ufanywe uhakiki wa watumishi hewa kwa sababu unaweza ukakuta hata wizarani wapo. Hili suala nitalifikisha kwa Waziri wa Utumishi,” alisema Simbachawene na kuongeza kuwa baada ya kukamilika itafikishwa mbele ya Rais Magufuli.

Aidha, aliwataka wakuu hao wa mikoa, kutambua mamlaka yao na kuyatumia ipasavyo ili kila aliyehusika kwa namna moja au nyingine katika watumishi hao hewa anachukuliwa hatua haraka ipasavyo. Awali, wakiwasilisha ripoti zao, baadhi ya wakuu wa mikoa walisema kuwa bado hawajapata idadi kamili ya fedha zilizopotea kutokana na idadi ya watumishi hewa katika mikoa yao.

Akiwasilisha ripoti yake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Daudi Ntibenda alisema wamebaini kuwepo kwa watumishi hewa 270 ambao wamesababisha hasara ya Sh bilioni 1.8 katika kipindi cha mwaka mmoja. Wengine waliowasilisha na idadi ya watumishi hewa kwenye mabano ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella (334). Alisema bado hawajapata idadi halisi ya hasara kutokana na watumishi hao kulipwa mishahara.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mathew Mtigume aliwasilisha (231) na hawajapata gharama halisi za fedha walizochota. Mikoa mingine iliyowasilisha ripoti na idadi ya watumishi hewa kwenye mabano ni Kigoma (171) hasara Sh milioni 104.6, Pwani (150) hasara bado haijapatikana, Dodoma (139) hasara ni Sh milioni 287 kwa kipindi cha miezi sita, Morogoro (122) hasara ni zaidi ya Sh milioni 450, Kilimanjaro (111) hasara Sh milioni 281.4
.
Mingine ni Tanga (104) hasara bado haijapatikana, Mbeya na Songwe (98) hasara ni Sh milioni 459.6, Mara (94) hasara Sh milioni 121, Dar es Salaam (73) hasara Sh milioni 316, Lindi (57) hasara Sh milioni 36.2, Tabora (38) hasara Sh milioni 118.7 na Ruvuma (37) hasara Sh milioni 58. Mkoa wa Simiyu (62) hasara Sh milioni 320, Njombe (34) hasara Sh milioni 20.1, Katavi (21) hasara Sh milioni 20.7, Manyara (50) hasara Sh milioni 42, Iringa (15) hasara haijapatikana na Kagera (14) hasara Sh milioni 49.1.

Akitoa siri ya mkoa wake kutokuwa na watumishi hewa, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anne Kilango Malecela alisema viongozi waliotangulia kabla yake, waliweka mikakati mizuri jambo lililowezesha wasiwepo watumishi hao. “Viongozi waliokuwepo walianza zoezi hili tangu mwezi Julai mwaka jana na kila tarehe 26 ya mwisho wa mwezi walikuwa wakihakiki watumishi wao hivyo ndio maana hakuna watumishi hewa,” alisema Anne- Kilango, ambaye katika Serikali ya Awamu ya Nne alikuwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri alisema katika mkoa wake yapo majina ya watumishi hewa, ambayo yapo katika orodha ya malipo ya mishahara, na kutoa mfano wa Manispaa ya Tabora peke yake hasara iliyotokana na kulipa watumishi hewa ni Sh milioni 24. Machi 15, mwaka huu wakati akiwaapisha Wakuu wa Mikoa, Rais Magufuli alitoa siku 15 kwa viongozi hao kuhakikisha wanajumuisha wafanyakazi wote na kuwaondoa watumishi hewa.

Aidha, juzi Rais Magufuli alisema uhakiki mdogo uliofanywa hivi karibuni kuhusu tatizo la wafanyakazi hewa nchini, umebaini wafanyakazi hewa 1,680 waliokuwa wakilipwa Sh bilioni 1.8. Alisema ni matarajio kuwa uhakiki unaofanywa nchi nzima, utaisaidia serikali kubaini wafanyakazi hewa wengi zaidi na kunusuru fedha nyingi zaidi za Watanzania.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Chato mkoani Geita juzi, Rais Magufuli alitoa mfano wa mfanyakazi mmoja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambaye alikuwa akilipwa mishahara ya watu 17, na kueleza kuwa mfanyakazi huyo atafikishwa mahakamani. Awali akifungua kikao cha kujadili bajeti inayopelekwa bungeni na utekelezaji wa bajeti iliyopita, Waziri Simbachawene aliwaagiza Wakuu wa Mikoa hao kuhakikisha wanasimamia vizuri elimu bila malipo.

“Lakini pia hakikisheni watumishi wanajituma na kuwafundisha wanafunzi vizuri ili kupata elimu bora. Kuna malalamiko mengi ya wananchi ambayo yanafika mpaka kwa Rais na baadaye ndio yanarudi kwa waziri na mkuu wa mkoa, tujitahidi kuhakikisha tunatatua migogoro katika hatua ya mwanzo,” alisema Simbachawene.
Aidha, aliwaagiza kushughulikia tatizo la mlundikano wa watumishi katika maeneo ya mijini kwani mlundikano huo hauna tofauti na watumishi hewa. Alisema kwa kada ya ualimu zipo shule ambazo zina idadi kubwa ya walimu kuliko mahitaji.

“Unakuta shule moja walimu wanaotakiwa ni 40 tu lakini unakuta 120 hadi wengine hawana kazi…kisingizio ni kwamba hela ya uhamisho wahamisheni sisi tutatoa hela ya uhamisho,” alisema Simbachawene. “Serikali za Mitaa katika maeneo yenu zizingatie kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, serikali imejipanga kuhakikisha inapunguza gharama za kujiendesha kwa kubana matumizi katika maeneo yasiyokuwa na tija,” aliongeza Simbachawene.
 
“Mamlaka zote zinasimamia jambo la ukusanyaji wa mapato kwa kuhakikisha ukusanyaji huo unafanyika kwa njia ya elektroniki, ambao unaonesha matokeo mazuri ni lazima uwe umeunganishwa katika mfumo wetu kwa sababu wapo watu wana zile mashine lakini hazijaungwa katika mfumo wetu,” alisema.

UPIMAJI WA MAENEO YA KILIMO NA UFUGAJI YAANZA KWA KASI

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi.

KATIKA kutekeleza agizo la Rais John Magufuli la kuona hatua zinachukuliwa za kumaliza migogoro baina ya wakulima na wafugaji, kazi ya kupima maeneo ili kutenganisha matumizi ya kilimo na ufugaji imeanza kwa kasi.

Hayo yalibainishwa Dar es Salaam jana wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, ilipotembelea ofisi za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA), ambayo imeanza kufanya kazi hiyo katika vijiji mbalimbali nchini.

Akiwaapisha Wakuu wa Mikoa hivi karibuni, Rais Magufuli alisema sababu kubwa iliyomfanya kumuondoa aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Rajabu Rutengwe ilikuwa ni kwa kiongozi huyo kushindwa kukomesha mapigano baina ya wakulima na wafugaji yaliyoshamiri mkoani humo.

Mratibu wa Mkurabita, Seraphia Mgembe akitoa maelezo mbele ya Kamati hiyo iliyoongozwa na Makamu Mwenyekiti wake, Mbunge wa Jimbo la Kavuu, Dk Pudensiana Kikwembe (CCM), alisema upimaji wa maeneo ya ardhi ni moja ya manufaa ya Mpango wa Mkurabita kwa Taifa.

“Ndugu Makamu Mwenyekiti uwepo wa mipango ya matumizi bora ya ardhi katika vijiji 96 umechangia kupunguza migogoro ya ardhi katika vijiji hivyo. “Katika maeneo yote tuliyopima tumefanikiwa kukomesha migogoro baina ya wakulima na wafugaji kwa kuoanisha maeneo ambayo ni kwa ajili ya wakulima tu na maeneo ambayo ni kwa ajili ya wafugaji tu, na wananchi wenyewe ndio wanaotusaidia katika kufikia uamuzi huo ambao unaheshimiwa na pande zote,” alisema Mgembe.

Pamoja na faida hiyo, Mratibu huyo alisema urasimishaji wa ardhi na biashara unaofanywa na Mkurabita pia umewezesha wamiliki 208 waliopewa Hati za Haki Miliki za kimila, kutumia hati hizo kama dhamana na kupata mikopo ya thamani ya Sh bilioni 2.4 na wakati huo huo vyama vitano vya wakulima vimepata mkopo wenye thamani ya Sh bilioni 4.7
.
 Kwa upande wa mjini, alisema wamiliki 93 waliorasimisha viwanja vyao mjini wametumia hati miliki zao kupata mikopo yenye thamani ya Sh bilioni 1.07